NDOTO ILIYOZIMIKA

Emakulata Msafiri

Mwanakwetukids

Ally alikuwa kijana mwenye ndoto kubwa tangu utotoni. Alitamani kuwa daktari maarufu. Kila alipomuona muuguzi au daktari wakihangaika kuwasaidia wagonjwa katika hospitali ya jirani moyo wake ulijawa na hamasa. Aliamini kuwa siku moja angevaa koti jeupe stethoscope shingoni na kuwahudumia watu kwa moyo wa huruma.

Shuleni Ally alipenda sana masomo ya sayansi . Walimu wake walimpongeza mara kwa mara kwa bidii yake. Marafiki zake walimwita “daktari wa kesho” kwa sababu kila alipokutana na mgonjwa alikuwa wa kwanza kushauri kwenda hospitali na mara nyingine hata kusaidia kwa msaada mdogo alioelewa.

Lakini safari ya elimu haikuwa rahisi. Baada ya kumaliza kidato cha nne Ally alipata matokeo ya wastani. Hayakumwezesha kuendelea na masomo ya sayansi katika shule ya sekondari ya juu. Ndoto yake ya kuwa daktari ikaanza kuyumba.


Alijitahidi mara ya pili kwa kujisomea na kurudia mtihani lakini changamoto za kifamilia zilimkabili. Baba yake aliugua kwa muda mrefu na Ally akawa ndiye tegemeo la familia. Ili kusaidia mama na wadogo zake.Ally alianza kufanya kazi ndogondogo mjini kubeba mizigo sokoni na hata kuuza bidhaa barabarani. Muda wa kusoma ukazidi kupungua na polepole ndoto yake ikaanza kufifia.

Miaka ilivyopita Ally alibaki akihisi maumivu moyoni. Kila alipomuona daktari akihudumia wagonjwa hospitalini macho yake yalijawa na huzuni. Aliwaza “Laiti ningepata nafasi zaidi ya kusoma huenda ningekuwa mmoja wao.”

Hata hivyo Ally hakuwahi kuacha kabisa moyo wa huruma. Alijiunga na kikundi cha vijana wanaojitolea kutoa msaada wa kwanza na elimu ya afya mitaani. Ingawa hakuwa daktari kama alivyoota bado alihisi anatimiza sehemu ya ndoto yake kwa kuwahudumia watu kwa moyo mweupe.

 

emakulatemsafiri@gmail.com

0653903872

 

 

 

0/Post a Comment/Comments