MSHINDI WA USIKU WA GIZA

Emakulata Msafiri

Kulikuwa na msichana mdogo aliyeitwa Naomi. Naomi alikuwa anapenda sana kuimba. Kila siku aliporudi nyumbani kutoka shuleni alikuwa anaenda nyuma ya nyumba na kuimba nyimbo zake anazozipenda.

Siku moja shule yao ilitangaza kutakuwa na shindano la kuimba. Naomi alifurahi sana na kuamua kushiriki. Alienda nyumbani na kuanza kujifunza nyimbo mpya. Kila siku alikuwa anafanya mazoezi lakini wakati mwingine alipokosea sauti alikuwa anakata tamaa na kusema:


 "Labda siwezi kushinda. Wengine wanaimba vizuri kuliko mimi."

Mama yake alimsikia na kumwambia: "Naomi usikate tamaa. Kila kitu kinahitaji mazoezi na uvumilivu. Ukiendelea kujaribu  utakuwa bora zaidi."

Naomi alisikiliza ushauri wa mama yake. Aliendelea kufanya mazoezi kila siku. Wakati washindano ulipofika Naomi aliogopa kidogo lakini alikumbuka maneno ya mama yake: "Usikate tamaa."

Alipopanda jukwaani  alichukua pumzi kubwa na kuimba kwa moyo wake wote. Sauti yake ilisikika vizuri na watu wote wakashangilia. Mwisho wa shindano Naomi alishinda nafasi ya kwanza!

Alirudi nyumbani akiruka kwa furaha na kumkumbatia mama yake. Tangu siku ile Naomi alijua kwamba hawezi kufanikiwa bila kujaribu na bila kuvumilia.

 


 

emakulatemsafiri@gmal.com

0653903872

 

 

 

 

 

0/Post a Comment/Comments