KUFUNDISHA WATOTO ADABU


Na, Emakulata Msafiri

Adabu ni msingi muhimu wa maisha ya binadamu. Katika jamii yoyote ile, mtu mwenye adabu huheshimiwa, hupendwa na huchukuliwa kuwa ni kielelezo chema kwa wengine. Kwa hivyo, ni wajibu wa kila mzazi, mlezi na mwalimu kuhakikisha kuwa watoto wanalelewa katika misingi ya adabu na maadili mema tangu wakiwa wadogo.

Watoto ni kioo cha familia na taifa kwa ujumla. Mtoto anayelelewa kwa adabu huwa na heshima kwa wakubwa, hutoa msaada kwa wadogo, na huishi kwa kuzingatia maadili ya jamii yake. Adabu ni kama taa inayoangaza njia ya mtoto, humwongoza katika kufanya maamuzi mazuri na kuepuka maovu.

Kufundisha watoto adabu kunaweza kufanyika kwa njia mbalimbali. Kwanza kabisa ni kwa njia ya mfano bora. Watoto hujifunza zaidi kwa kuiga matendo ya wazazi wao au walezi. Ikiwa mzazi anatumia lugha nzuri, husalimia watu, na huonyesha upendo na heshima kwa wengine, basi mtoto naye atafuata mfano huo.


Pili, watoto wanapaswa kufundishwa
maneno ya heshima kama vile “tafadhali”, “asante”, “samahani” na “pole”. Maneno haya huonyesha adabu na huwasaidia kuwasiliana vizuri na watu wengine katika jamii. Mzazi au mwalimu anapaswa kuwasisitizia watoto kutumia maneno haya kila siku hadi yawingie katika maisha yao ya kawaida.

Tatu, ni muhimu kuwafundisha watoto thamani ya kusikiliza na kuheshimu wakubwa. Katika jamii nyingi, mtoto anayejibu watu wazima au anayekatiza mazungumzo bila ruhusa huchukuliwa kuwa hana adabu. Hili linaweza kufundishwa kwa kuwaeleza watoto madhara ya tabia hizo na kuwapa mbinu sahihi za kuwasiliana.

Hata hivyo, kuna changamoto nyingi katika kufundisha watoto adabu. Baadhi ya wazazi hawana muda wa kutosha wa kukaa na watoto wao. Vilevile, maendeleo ya kiteknolojia kama vile runinga na simu yamechangia watoto kuona tabia zisizofaa ambazo huathiri malezi yao. Kwa hivyo, ni muhimu kwa wazazi kuweka mipaka ya matumizi ya vyombo vya habari na kuhakikisha watoto wao wanapata maudhui yenye maadili.

 


 

emakulatemsafiri@gmail.com

0653903872

0/Post a Comment/Comments